TANGAZO
Wakati dirisha la usajili likiwa bado halijafunguliwa rasmi na Shirikisho la Soka Tanzania, Klabu ya Simba imeendelea kufanya usajili wake baada ya juzi jioni kuwasainisha mikataba wachezaji wapya wawili ambao wote ni mabeki, Mohammed Fakhi kutoka JKT Ruvu na Samir Haji Nuhu ambaye aliwahi kuichezea Azam FC.
Kwa mujibu wa habari zilizopatikana jijini jana zinaeleza kuwa Fakhi ambaye pia ana Diploma ya IT aliyoipata katika Chuo cha Learn IT cha jijini Dar es Salaam na Nuhu, kila mmoja amesaini mkataba wa kuichezea klabu hiyo yenye Makao Makuu mtaa wa Msimbazi, Kariakoo jijini Dar es Salaam kwa kipindi cha miaka miwili.
Akizungumza na gazeti hili baada ya kukamilisha usajili huo, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Wekundu wa Msimbazi, Zacharia Hanspoppe, alisema wanatarajia usajili huo utaimarisha safu yao ya ulinzi na hatimaye kutoruhusu mabao kwenye msimu ujao wa ligi.
Hanspoppe alisema wamemalizana na wachezaji hao na mara muda wa mazoezi kwa ajili ya maandalizi ya msimu ujao utakapofika, wataungana na nyota wengine kuanza kujifua.
Fakhi aliwaahidi mashabiki wa Simba kuitumikia klabu hiyo kwa uadilifu na kwa kucheza katika kiwango cha juu.
Alisema anafahamu wazi kuwa akifanya vizuri ndani ya Simba anaweza kupata timu nyingine ndani au nje ya nchi ambayo itamlipa maslahi bora zaidi.
"Mpira ni kazi yangu na moja ya mafanikio ni kusajiliwa kwenye klabu kongwe, nimeipata hii nafasi lakini naamini nastahili kusonga mbele zaidi kutokana na uwezo nilionao," alitamba beki huyo ambaye pia anaichezea timu ya Taifa ya Zanzibar (Zanzibar Heroes).
Naye Rais wa Simba, Evans Aveva, aliongeza kuwa bado wanaendelea na mchakato wa kusaka kocha mkuu ambaye atakuja kurithi mikoba ya Mserbia Goran Kopunovic.
Aveva alisema hawataki kukurupuka kwenye maamuzi ya nani awe Kocha Mkuu kwa sababu malengo yao ni kupata kocha atakayeweza kufanya kazi kama matarajio yao yalivyoanishwa kwenye vipengele vya mkataba.
"Bado tuko kwenye mchakato, hatujafikia mwisho," alisema kwa kifupi rais huyo.
TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by TeachMaker
Post a Comment